Zinedine Zidane amefunguka kuhusu tetesi za uwezekano wa mchezaji wa Manchester United, Paul Pogba kujiunga na Real Madrid kupitia neema ya usajili wa vitita vizito unaotajwa kufanywa na kocha huyo.

Zidane amesema kuwa anasikia yote yanayozungumzwa kuhusu Pogba na safari ya kuelekea Madrid lakini amezitaja taarifa hizo kuwa ni upuuzi ambao hataki kujihusisha nao.

“Pogba ni mchezaji mzuri, mchezaji ninayemfahamu, lakini ni hivyo tu. Sitaingia kwenye mambo hayo, hayo ni upuuzi,” amesema Zidane.

“Kama utaniuliza mimi kuhusu Pogba, nitakwambia ni mchezaji wa Manchester United. Ni mchezaji mzuri lakini ni wa Manchester United,” aliongeza.

Alisema kuwa watafahamu zaidi kitakachotokea baada ya msimu kuisha.

Katika hatua nyingine, Zidane amewashusha presha mashabiki wa Real Madrid wenye kiu ya kuona usajili utakavyofanyika akiwaeleza kuwa huenda suala la usajili mkubwa likafanyika au lisifanyike wakati huu.

RC Mwangela atoa agizo kuhusu Dampo
Kikwete ataka habari za mtandaoni kifo cha Dkt. Mengi zipuuzwe, awataja wanaoujua ukweli