Msanii wa kike ambaye alikuwa mwanafamilia wa kundi la Wakilisha, Witnesz leo amesimulia kisa na mkasa wa kuvunjika kwa kundi hilo lililokuwa linaundwa na yeye, Sara na marehemu Langa.

Mkali huyo wa michano ambaye siku hizi huimba pia, ameiambia East Africa Radio kuwa sababu kuu ya kuvunjika kwa kundi hilo ilikuwa pesa na kwamba walibaini meneja wao alikuwa anawaibia kiasi kikubwa cha fedha kwa udanganyifu.

Amesimulia kuwa walishtuka walipoambiwa kuwa hulipwa hadi  Sh5 Milioni (5,000,000) kwa onesho (show) moja, kiasi ambacho kilikuwa kikubwa kwa wakati huo, lakini meneja wao alikuwa anawadanganya kuwa hulipwa Sh300,000 tu na kwamba bado kuna asilimia kadhaa hutumwa Afrika Kusini kwa walioandaa shindano la Coca-Cola Pop Stars.

Sara, Witnez na Langa (Wakilisha) 

“Tuligundua kuwa hakuna fedha ambayo ilikuwa inatumwa Afrika Kusini, na angalia kwa wakati ule kumbe tulikuwa tunapiga show hadi kwa Sh5 milioni. Lakini meneja alikuwa anapiga zote anatuambia tumelipwa Sh300,000 tu,” alisema Witnesz huku akisisitiza kuwa meneja huyo sio Master Jay.

Rapa huyo ambaye hujiita pia Kibonge Mwepesi alisema kuwa baada ya kugundua hilo, pamoja na mambo mengine, waliamua kila mmoja apambane kivyake.

Witnesz anafanya muziki kwa ukaribu na mpenzi wake Ochu Sheggy na moja kati ya nyimbo zao zilizopata umaarufu hivi karibuni ni ‘Jirani’ waliomshirikisha Snura na Mzee Yusufu.

Video: Wizara ya maliasili na utalii yaandaa tamasha la kuenzi utamaduni wa mtanzania
Diamond: Hii ndio starehe yangu kubwa