Mahakama Kuu ya Tanzania imewahukumu askari Polisi wawili wa kutoka kituo cha Oysterbay jijini Dar es Salaam na watu wengine sita kwenda jela miaka 35 kwa makosa mawili ya kukutwa nyara za serikali na kujihusisha na mtandao wa ujangili.

Hayo yamesemwa na Wakili wa Serikali, Salimu Msemo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma, ambapo aliwataja polisi hao wa zamani waliokutwa na hatia ni wenye namba D 8656 CPL Senga Nyembo na G 553 PC Issa Mtama washtakiwa walikutwa na meno 70 ya tembo yenye thamani ya Sh. milioni 800.

Wengine sita waliokuwa nao wote wamekutwa na hatia ni pamoja na Prosper Maleto, Seif Mdumuka, Amri Bakari, Said Mdumuka, Ramadhan Athuman na Musa Mohamed.

Aidha, amesema kuwa washtakiwa hao walikutwa na kosa hilo katika eneo la kituo cha ukaguzi cha Kauzeni lililopo Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani kabla ya kufikishwa kortini na kukumbana na adhabu hiyo.

Hata hivyo, ameongeza kuwa katika kosa la kwanza, washtakiwa walihukumiwa kwenda jela miaka 20 kila mmoja na faini kwa kila mmoja, wakati katika kosa la pili, washtakiwa wawili ambao ni hao polisi, walihukumiwa miaka 15 kwenda jela.

Majaliwa atoa onyo kali kwa viongozi Serikalini
Hamiliton azidi kung'ara mbio za Singapore Grand Prix