Waziri wa Biashara nchini Kenya, Peter Munya amehojiwa katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) nchini humo kwa madai ya kupanga njama za kumuua Makamu wa Rais, William Ruto.

Waziri huyo alihojiwa pamoja na wenzake wawili ambapo walidaiwa kufanya vikao va siri vyenye lengo la kupanga mauaji.

Kwa mujibu wa Daily Nation, Munya amezungumza na waandishi wa habari nje ya ofisi za Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai na kukana tuhuma hizo dhidi yao.

Hata hivyo, Munya alikiri kuwa walifanya vikao kadhaa lakini hawakuwa wanapanga njama au kumzungumzia Makamu wa Rais.

“Hakujawahi kuwa na vikao vyovyote vya kujadili kuhusu kumuua, kumdhuru au hata kumzungumzia tu Makamu wa Rais kwa nia ovu,” The Standard wamemkariri Munya.

Waziri wa Biashara wa Kenya, Peter Munya

Alisema kuwa DCI aliwaeleza kuwa amewaita kwa sababu Makamu wa Rais alimpigia simu na kutoa malalamiko yake kuhusu vikao hivyo vinavyoendelea kati yao.

“DCI alituthibitishia kuwa Ruto alimpigia simu na kulalamika na alitaja Mei 14, 2019 kama siku ambayo tulikutana pia,” alisema Munya.

Tuhuma hizo zilizua gumzo zaidi nchini humo kutokana na mpango wa wazi wa Ruto kuwa atagombea Urais mwaka 2022.

Joto la uchaguzi huo limezua mambo mengi nchini Kenya huku ndani ya Serikali ya Rais Uhuru Kenyatta kukiwa na makundi kadhaa ya wanaotaka kuwania urais.

Pierre, Wabunge warejea nchini kimyakimya, 'Unataka kuilaumu Stars, Senegal wanamishahara mikubwa'
Vita ya Nicki Minaj na Miley Cyrus yafika pabaya