Watu 12 wameuawa na wengine sita wamejeruhiwa katika ufyatulianaji wa risasi uliofanyika katika jumba la serikali jimbo la Virginia nchini Marekani.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na maafisa wa polisi zinaeleza kuwa mshukiwa wa mauaji hayo ni mfanyakazi wa muda mrefu katika kituo cha manispaa ya Virginia.

Mshukiwa huyo ambaye jina lake bado halijatajwa alifyatua risasi kiholela lakini baadaye aliuawa baada ya polisi kuwasili katika eneo hilo na kumkabili.

Afisa mkuu wa polisi James Cervera amesama jana majira ya saa kumi walipata taarifa za ufyatuliaji risasi na katika makabiliano naye afisa mmoja alijeruhiwa.

“Afisa mmoja wa polisi ni miongoni mwa wale waliojeruhiwa baada ya risasi kupiga nguo yake ya kuzuia risasi” ameeleza afisa Cervera

Aidha maafisa wa polisi wamesema wanaamini kwamba mshambuliaji huyo alikuwa peke yake na lengo la mtu huyo bado halijatambuliwa.

Baada ya shambulio eneo hilo lenye majumba mengi ya serikali lilifungwa na wafanyakazi wa Serikali kuondolewa.

Gavana wa Virginia Ralph Northam amesema kuwa haya ni maafa mabaya kwa wakazi wa Virginia kuwahi kutokea.

Maafisa wa Ujasusi wa FBI walikuwa katika eneo hilo kuwasaidia maafisa wa serikali za mitaa kuchunguza shambulio hilo

Kwa mujibu wa mtandao wa Marekani wa Gun violence Archive hili ni shambulio la 150 kufanyika nchini Marekani mwaka huu.

 

 

Watanzania 10,000 kupata ajira mradi wa bomba la mafuta ghafi
Video: Ufahamu ugonjwa wa Ini hatari zaidi ya Ukimwi, hauna tiba, dalili, maambukizi