Serikali imewafikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu watu watatu kwa kosa la kukutwa na tausi watatu wanaodaiwa kuwa wa Ikulu.

Washtakiwa hao ni David Graha, Mohamed Hatibu na Mohamed Ally, wamefikishwa mahakamani hapo leo Ijumaa Oktoba 25, mbele ya Hakimu Mkazi Vicki Mwaikambo.

Wakili wa serikali Mkuu Faraja Nchimbi akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi Wankyo Simon, wamedai washtakiwa hao walitenda makosa hayo kati ya Julai Mosi mwaka 2015 hadi Oktoba 14, mwaka huu jijini Dar es Salaam

Inadaiwa kuwa katika kipindi hicho, washtakiwa hao walijihusisha na kuratibu mtandao wa uhalifu kwa kujihusisha na biashara ya ndege aina ya tausi bila kuwa na kibali kutoka kwa Mkurugenzi wa Wanyamapori.

Ambapo imedaiwa katika kipindi hicho, washtakiwa walikutwa na tausi watatu wenye thamani ya Dola za Marekani 1500 sawa na Sh 3,444,150 mali ya serikali bila ya kibali.

Baada ya kusomewa mashtaka hayo, Hakimu aliwataka Washtakiwa hao kutojibu lolote kwakuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.

Kesi itatajwa tena Novemba 7 mwaka huu.

Wakandarasi wakichina waliolala rumande usiku mmoja waachiwa kwa dhamana
Wadaiwa sugu waundiwa mfumo wa kuwadhibiti