Wananchi Wilayani Uyui mkoani Tabora Wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwawezesha kurasimisha mashamba yao na kupatiwa hati za haki milki za kumiliki ardhi hali inayowawezesha kujikwamua kiuchumi.

Baadhi ya wananchi hao wakizungumza wakati wa mahojiano maalum Wilayani humo akiwemo mkazi wa Miyenze Bw. Julius Magoi amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imeonesha dhamira ya dhati kuwawezesha wananchi Vijijini kupitia Mpango wa Kurasimishaji Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA).

“Tunamshukuru Rais Magufuli kwa kuwezesha MKURABITA kuturasimishia mashamba yetu, kuyapima na kupatiwa hati za haki milki za kimila hali inayotuwezesha kuongeza tija katika uzalishaji mashambani hasa katika mazao ya biashara” Amesema Magoi

Akifafanua amesema kuwa MKURABITA imeendesha mafunzo yanawawezesha wakulima kuendana na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano kuwakwamua wananchi wanyonge hasa wanaoishi vijijini katika Wilaya hiyo kwa kuwajengea stadi za kilimo bora, ufugaji wa kuku kibiashara, kilimo cha pamba, alizeti na mazao mengine .

Kwa upande wake mkazi mwingine wa Kata hiyo, Nyamizi Shija amesema kuwa anamuomba Rais Magufuli aendelee na jitihada zake za kuwawezesha wananchi kama ambavyo anafanya sasa kwa kuwa wanaendelea kumuunga mkono katika kila jambo analofanya ili kuwaletea maendeleo.

Naye Meneja Urasimishaji Ardhi Vijijini kutoka MKURABITA, Antony Temu amebainisha kuwa wananchi wa Kata za Miyenze na Lutende wamejengewa uwezo wa kutekeleza kilimo chenye tija cha mazao ya biashara kama alizeti, pamba na mengine ili waweze kuzalisha kwa tija.

Mafunzo ya kuwajengea uwezo wananchi waliorasimisha mashamba yao na kupatiwa hati za hakimilki za kimila yamefanyika katika Kata ya Miyenze na Lutende Wilayani Uyui mkoani Tabora na kushirikisha wakulima zaidi ya 200.

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Mei 19, 2019
Mwalimu kuburuzwa mahakamani kwa tuhuma za rushwa