Kampuni ya ulinzi ya G1 inayolinda hoteli ya Colosseum jijini Dar es Salaam imetoa taarifa inayoeleza sababu za walinzi wake kutokuwa na bunduki au bastola wakati bilionea Mo Dewji alipotekwa Oktoba 11 mwaka huu katika hoteli hiyo.

Taarifa ya kampuni hiyo imeeleza kuwa mkataba wake na hoteli hiyo hauruhusu walinzi wake kuwa na silaha za moto, na kwamba siku zote wamekuwa wakiilinda hoteli hiyo bila silaha za moto ikiwa ni matakwa ya mteja wao.

“Mteja anapokuja sisi tunamwambia tuna alarm, mbwa na silaha. Tunaorodhesha package tulizonazo, kwa hiyo mteja atachagua na hatuwezi kumlazimisha atumie silaha,” Mwananchi inamkariri kiongozi wa kampuni ya G1 aliyejitambulisha kama Magwila.

Alisema kuwa hoteli hiyo ilichagua kulindwa bila silaha za moto na kwamba wakati wa tukio hilo kulikuwa na walinzi watano waliokuwa zamu ambao hivi sasa wanashikiliwa na jeshi la Polisi.

Aidha, Magwila alisema kuwa mkataba wao na mteja wao huyo hauwaruhusu kusimamia camera za CCTV zilizofungwa.

Jana, familia ya Mo Dewji ilitangaza zawadi ya Sh1 bilioni kwa mtu atakayetoa taarifa zitakazosaidia kupatikana kwa mtoto wao.

Afisa usalama wa taifa Kenya akamatwa na ‘unga’
Trump adai huenda mwandishi aliyetoweka aliuawa na Wahuni