Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa amesema Jeshi hilo limewakamata wafanyakazi hao kwa tuhuma za wizi wa Dola za Marekani 402,000 (Tsh. 1,280,000,000) na Yuro 27,700 (Tsh. 69,320,048).

Waliokamatwa ni Dereva wa G4S, Christopher Cleophace Rugemalira (34), Mlinzi wa G4S, Mohamed Athuman Ramadhan (40), Mlinzi wa G4S, Ibrahim Ramadhan Maunga (49) na Salimu Shamte (45).

Mambosasa amesema Februari 17, 2020, Watuhumiwa Christopher, Mohamed na Ibrahim walipewa fedha kutoka tawi la benki ya NBC Kariakoo na NBC Samora wazipeleke Makao Makuu ya NBC, lakini hawakufanya hivyo na walienda Temeke Maduka Mawili ambapo walipanda gari jingine lililokuwa likiendeshwa na Salimu Shamte.

Baada ya Polisi kupata taarifa, walianza uchunguzi ambapo Mtuhumiwa Christopher alikamatwa Mongo la Ndege na alikutwa na Tsh. 110,000,000 pamoja na magari matano aina ya BMW, Toyota Runx na Toyota IST (3).

Pia, Mtuhumiwa alikiri kuwa ameshanunua nyumba mbili na kiwanja vyenye thamani ya Tsh. 107,000,000, samani za Tsh. 5,000,000 na kufanya jumla ya mali na fedha taslimu kuwa Tsh. 297,110,000.

Februari 21, 2020 watuhumiwa Mohamed na Salimu walikamatwa huko Mbagala na walikutwa na Tsh. 332,000,000 na Yuro 5,010 na gari aina ya Toyota IST. Pia walikiri kununua viwanja maeneo ya Kisemvule na Kivule vya thamani ya Tsh. 25,000,000.

Aidha, Februari 24, 2020 Mtuhumiwa Ibrahim alikamatwa na alikutwa na Tsh. 195,213,450 na pia alikiri kununua nyumba Kibaha ya Tsh. 30,000,000 na samani za ndani za thamani ya Tsh. 10,000,000.

Tanzania kunufaika na soko la viungo Uswisi
Rais wa zamani wa Misri afariki dunia