Wakuu wa Wilaya wametakiwa kusimamia zoezi la kuhakiki idadi ya wakulima wa tumbaku na ukubwa wa mashamba ambayo wanaweza kulima kwa ajili ya kuweka mipango ya uagizaji wa pembejeo kulingana na mahitaji halisi.

Agizo hilo limetolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa mjini Tabora wakati wa kikao cha majumuisho ya ziara ya siku nne mkoani hapo.

Amesema kuwa lengo ni kutaka kuboresha uzalishaji wa zao hilo na kuweka mazingira ambayo mkulima hataendelea kunyonywa na baadhi watu ambao hawalimi tumbaku lakini ikifika wakati wa uuzaji wanajifanya nao ni wakulima wa tumbaku.

Aidha, Majaliwa ameongeza kuwa hatua hiyo pia itasaidia wataalamu wa eneo husika kuweza kujua kwa haraka mahitaji ya wakulima wa zao la tumbaku katika eneo lake na hivyo kuwasaidia ili waweze kuzalisha kwa wingi na tumbaku iliyo katika kiwango bora.

Vile vile amesisitiza kuwa msimamo wa Serikali ni kuwa kila mkulima atauza tumbaku yake kupitia Chama cha Msingi na atapaswa awe amesajiliwa na Chama kilichopo katika eneo lake na sio vinginevyo.

Hata hivyo, amesema kuwa kinyume cha hapo mtu yoyote awe Mwanasiasa au mtumishi wa umma atakayekamatwa anajihusisha na ununuzi wa tumbaku au uuzaji wa pembejeo za kilimo kinyume na maelekezo ya Serikali atakamatwa na  hatua kali dhidi yake zitachukuliwa.

 

Video: Meya wa Kinondoni kujenga stendi ya Daladala Kawe
Christian Bella akumbuka msoto wa kujiunga na bendi ya Koffi , sasa anatafutwa