Mbunge wa Jimbo la Ukonga kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Mwita Waitara amekihama chama hicho na kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Waitara amesema sababu kubwa ni kutofautiana na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe baada ya kumhoji kwa nini chama hicho hakifanyi uchaguzi wa mwenyetiki wa chama Taifa.

Amesema kuwa ukiwa ndani ya Chadema hauruhusiwi kuhoji chochote na endapo utahoji basi utaitwa msaliti ndani ya chama hicho.

Ameyasema hayo katika ofisi ndogo za CCM Lumumba jijini Dar es salaam alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuhama Chadema.

“Mimi ugomvi wangu na Mbowe, ni pale nilipohoji ni kwanini uchaguzi wa mwenyekiti haufanyiki ndani ya Chadema, hapo ndipo nikaanza kusakamwa na kuitwa msaliti, na kaniambia atanishughulikia, wakati huo hata Chacha Wangwe alimwambiaga hivyo na leo Wangwe hatuko naye,”amesema Waitara

Aidha, Waitara ametaja sababu nyingine iliyomfanya kukosana na Mbowe ni baada ya kuhoji hela za ruzuku milioni 236 ambazo huwa zinatolewa kila mwezi, lakini hazieleweki zinaelekea wapi, huku chama hicho kikiwa hakina Ofisi za Makao Makuu, Kanda wala Ofisi za Mikoa.

Hata hivyo, Waitara ameongeza kuwa kwasasa amejivua rasmi uanachama wa Chadema na kujiunga na chama cha mapinduzi CCM sehemu ambayo amedai kuwa ni salama.

Klopp ajibu kejeli za Mourinho, amtaja kwenye malengo yake
Mke amhubiria mumewe kwenye baa kuacha pombe