Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Geita imewafikisha Mahakamani maafisa wawili kati ya watatu kwa makosa ya kuomba na kupokea rushwa kinyume na sheria.

Hiyo imekuja siku chache mara baada ya wafanyabiashara nchini kukutana na Rais, Dkt. John Magufuli na kumweleza madudu yanayofanywa na baadhi ya watumishi wa mamlaka ya mapato Tanzania TRA.

Kwa mjibu wa Naibu Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Geita, Mwamba Masanja waliofikishwa Mahakamani ni pamoja na mshitakiwa wa kwanza, Sadick Kassim Lutenge na Elias Samwel Msula wote kwa pamoja wakituhumiwa kuomba rushwa ya zaidi ya Tsh. million 100, huku mshitakiwa wa pili Hamza Rugemalira akiendelea kutafutwa.

Awali, mbele ya Hakimu Mfawidhi Mkazi wa Mahakama hiyo, Jovit Kato, Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Kelvin Murusuri ameieleza Mahakama hiyo kuwa washitakiwa wa kwanza na wa pili wakiwa katika utekelezaji wa majukumu yao kwa pamoja walimuomba rushwa, Alphonce John Mirigo kiasi cha Tshs 30,000,000 ili waweze kufanya makadirio ya chini ya kodi ya biashara ya mfanyabiashara huyo.

Pia tarehe 4/6/2019 mshitakiwa wa kwanza alipokea kiasi cha tshs 10,000,000 ikiwa ni sehemu ya kiasi walichoomba, ambapo amesema, katika kipindi cha kati  ya tarehe  1/2/ 2019 na tarehe 30/4/2019 mtuhumiwa wa kwanza na wa tatu kwa pamoja waliomba kiasi cha Tsh. 75,000,000 kutoka kwa Bertha Charles Magandula na Makoye Athumani Shiyunga ambao ni wakurugenzi wa Makoye Hospital Co Limited na kwamba mnamo tarehe 8/4/2019 watuhumiwa kwa pamoja walipokea kiasi cha Tsh. 50,000,000 ikiwa ni sehemu ya fedha za rushwa walizoziomba kutoka kwa Bertha na Makoye.

Pia mnamo tarehe 14/6/2019 mshitakiwa wa tatu alijaribu kupokea kiasi cha tsh. 10,000,000 ikiwa ni sehemu ya fedha za rushwa ya kiasi cha Tsh. 30,000,000 alizoziomba kwa Alphonce.

Washitakiwa wote wamenyimwa dhamana kwa kuwa sheria ya uhujumu uchumi inazuia kwani thamani ya kiasi walichoomba ni zaidi ya milioni kumi.

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Juni 20, 2019
Video: TACIP yadhamini safari ya Pierre Misri, akabidhiwa tiketi bungeni