Teknolojia inaendelea kuziweka rehani baadhi ya kazi zinazofanywa na idadi kubwa ya binadamu, ambapo jana Dubai imezindua rasmi roboti ya polisi iliyoanza kufanya kazi mitaani ikiwasaka wahalifu na kupokea ripoti.

Roboti hiyo iliyofungiwa mfumo wa kielekroniki na kompyuta inaweza kurekodi picha za video na kuzituma kwenye vituo vya polisi, kupanga faini, kubaini sura za watu, huku ikizungumza lugha tisa tofauti.

Serikali imesema imebaini kuwa mfumo huo wa kutumia roboti ni mzuri na kwamba kufikia mwaka 2030 mfumo wa roboti utachukua asilimia 25 ya jeshi la polisi.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa kitengo cha huduma bora wa Polisi Dubai, Brig Khalid Al Razooqi amesema kuwa roboti haitachukua nafasi ya binadamu katika vitengo vya polisi.

“Nafasi za Polisi hazitachukuliwa na roboti. Lakini kwakuwa idadi ya watu wa Dubai inaongezeka, tunahitaji kuwapangia maafisa wa polisi maeneo mengine ili wajikite katika kuhakikisha hali ya usalama kwenye jiji,” alisema Razooqi.

Aliongeza kuwa wananchi wanaweza kuripoti matukio ya kihalifu kupitia kompyuta maalum iliyoko kwenye kifua cha roboti hiyo kwa kutumia lugha tisa tofauti.

Dubai ilianza kufanya utaratibu wa kuwa na mfumo wa polisi wa roboti tangu mwaka 2011, lakini sasa wamejihakikishia kuwa wanaweza kuwa na aina hiyo ya polisi.

Nukuu ya Leo
Chadema Waifuata CCM Dodoma, Wapanga Kuteta haya