Meya wa jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita amekabidhi Kompyuta mpakato (Laptop) 18 kwa shule tatu jijini humo ambazo ni shule ya Kambangwa iliyopo halmashauri ya Kinondoni, shule ya Kitunda iliyopo Ilala pamoja na shule Minazini iliyopo Kigamboni ambapo kila shule moja imepatiwa Komyuta sita.

Akizungumza katika hafla hiyo, amesema kuwa Kompyuta hizo zimefadhiliwa na Kampuni ya bia ya TBL, ambapo amesema zitakuwa msaada mkubwa kwa wanafunzi kujifunza masomo hayo ya sayansi ya Kompyuta.

Amesema kuwa jiji la Dar es salaam lina shule nyingi za Sekondari, lakini shule ambazo zimepatiwa ufadhili huo ni baadhi ya zile ambazo tayari zina madarasa ya kujifunzia kompyuta na kwamba ofisi yake kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itaendelea kutoa misaada mbalimbali

“Tunataka wanafunzi wetu wajifunze kulingana na wakati tulionao, ofisi yangu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali watakaoshirikiana nasi itaendelea kusaidia shule nyingine,”amesema Mwita.

Aidha ameiomba Kampuni ya TBL kuendelea kusaidia shule ili wanafunzi waweze kujifunza masomo hayo, huku akitoa wito kwa kampuni nyingine kuzisaidia shule kupata Kompyuta.

Kwa upande wake Meneja wa masuala endelevu wa TBL, Irine Mutiganzi amesema kuwa kampuni hiyo imekuwa ikijitoa katika maeneo mbalimbali ya kijamii na kwamba kwa kushirikiana na Meya Mwita wameona kuna haja ya kuzisaidia shule kuwapatia kompyuta.

Naye Mkuu wa shule ya Sekondari Kambangwa, Elestina Chanafi na Fulgence Daudi wa shule ya Sekondari Minazini wamemshukuru Meya wa jiji pamoja na TBL kwa kuweza kutoa msaada wa Kompyuta hizo.

Papa Francis: Messi sio Mungu
JPM kuiunganisha mikoa ya kusini, 'Hatuwezi kushindwa'