Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa anatarajia kuwa mgeni rasmi katika Uzinduzi wa Vituo 51 vya Hali ya Hewa vinavyojiendesha vyenyewe, Vituo 15 vya Kupima wingi wa maji Mtoni, Kanzidata ya Taarifa za Hali ya Hewa pamoja na Kituo cha Operesheni na Mawasilino ya Dharura.

Uzinduzi huo utafanyika Jumatano, tarehe 27 Juni, 2018 katika Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Bahi Jijini Dodoma, ambapo shughuli hiyo itarushwa mubashara na vyombo vya habari kuanzia saa sita mchana.

Akizungumza wakati wa maandalizi ya Uzinduzi huo Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu), Jenista Mhagama pamoja na kuwakaribisha wananchi wote kushiriki katika uzinduzi huo, amebainisha kuwa Kuzinduliwa kwa vituo hivyo, kanzidata na kituo cha Operesheni na Mawasiliano nchini ni baadhi ya jitihada zinazofanywa na Serikali ya awamu ya tano kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuhakikisha menejimenti ya maafa inaimarika nchini.

“Vituo hivyo vitawasaidia Watanzania ambao ni wadau wakubwa wanaotumia Taarifa za Hali ya Hewa katika kupata taarifa za awali za utabiri wa uwepo wa majanga au kutokuwepo ili kujiandaa, kuyakabili endapo majanga yatatokea pamoja na kusaidia katika maandalizi ya shughuli za maendeleao ikiwemo upatikanaji wa taarifa za hali ya hewa kusaidia kupanga aina za mazao yanayofaa kulimwa kulingana na mabadiliko ya tabia nchi”, amesema Mhagama

Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Mradi wa Kuimarisha Taarifa za Mabadiliko ya Tabianchi na Uboreshaji wa Mifumo ya Tahadhari za Awali, imeweza kuimarisha miundombinu na mazingira ya kufuatilia taarifa za mabadiliko ya tabianchi na kutengeneza mifumo imara ya kutoa tahadhari za awali, usimamizi wa maafa na kuchangia katika mipango ya maendeleo endelevu.

Mradi wa Kuimarisha Taarifa za Mabadiliko ya Tabianchi na Uboreshaji wa Mifumo ya Tahadhari za Awali, Uliandaliwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Tanzania na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) na kufadhiliwa kupitia Mfuko wa Uboreshaji wa Mazingira Duniani (GEF).

Mradi umetekelezwa na Wizara na Taasisi za Serikali ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Wizara ya Kilimo na Mamlaka ya Hali ya Hali ya Hewa Tanzania, tangu mwaka 2014 hadi Juni mwaka 2018.

SSC Napoli Kumng'oa Mateo Kovacic Santiago Barnabeu
Jeshi la polisi lasitisha maombi ya ajira