Uongozi wa klabu bingwa nchini Ufaransa Paris Saint-Germain, umemtangaza Thomas Tuchel kuwa meneja wa klabu hiyo, kwa kipindi cha miaka miwiwli ijayo.

Tuchel raia wa Ujerumani, amekamilisha mpango wa kujiunga na PSG, baada ya kukiongoza kikosi cha Borussia Dortmund kuanzia mwaka 2015 hadi 2017, na sasa anachukua nafasi ya Unai Emery, ambaye mkataba wake umefikia kikomo.

Tuchel hakuwahi kufanya kazi zozote za ukufunzi wa soka tangu alipoondoka Dortmund mwishoni mwa msimu 2016-17, baada ya kuiwezesha klabu hiyo kutwaa ubingwa wa kombe la Ujerumani, huku ikimaliza katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ya Ujerumani.

Meneja huyo mwenye umri wa miaka 44 atakua na shughuli ya kufanya makubwa zaidi ya waliomtangulia, hususan kuifikisha mbali PSG kwenye michuano ya ligi ya mabingwa barani Ulaya, baada ya msimu uliopita kufika hatua ya 16 bora na kutolewa na Real Madrid.

Baada ya kutambulishwa kuwa meneja wa kikosi cha PSG Tuchel alisema: “Ni furaha isiyo na kifani kwa upande wangu, maana nimetimiza lengo nililolikusudia kwa kipindi kirefu, najua kazi itakua kubwa kwangu na kwa wengine klabuni hapa, lakini ushirikiano baina yetu utaweza kutufikisha panapokusudiwa.”

Jorge Sampaoli atangaza jeshi la Argentina
Sheria yawabana wanandoa Kenya, Hakuna kugawana 50/50