Mwenyekiti wa baraza la vyama vya soka Afrika mashariki na kati, (CECAFA), Leodegar Chilla Tenga amesema hatagombea tena nafasi hiyo baada ya kumaliza muda wake mwishoni mwa mwaka.
Akizungunza mjini Brazzaville katika sherehe za kufunga Michezo ya Afrika juzi, Tenga amesema hatagombea tena, kwani ni wakati mwafaka sasa CECAFA kupata kiongozi mpya.
Tenga aliyezipongeza Sudan wanaume na Tanzania wanawake kuwa timu pekee zilizowaikilisha CECAFA katika michezo hiyo, amesema kwamba pamoja na kung’atuka ataendelea kuwa bega kwa bega na CECAFA kusaidia maendeleo ya soka ukanda huu.
“Wakati wote nimekuwa nikiachia madaraka baada ya kumaliza muda wangu. Niliondoka TFF na sasa natumai ni wakati sisi wa CECAGA kuchagua mtu mwingine pia. Mtu mmoja muwajibikaji na mwenye uwezo wa kutupeleka juu. Na lazima tumuunge mkono mtu sahihi,”amesema Tenga akizungumza na voiceofsport.net.
Aidha, Tenga amempigia debe Katibu wake, Mkenya Nicholas Musonye aendelee na nafasi hiyo kwa sababu ni mchapakazi hodari na anayejituma.
Uchaguzi wa CECAFA unatarajiwa kufanyika sambamba na michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, Challenge nchini Ethiopia katikati ya Novemba.

 

Unachopaswa Kufanya Unapoandamwa Na Tatizo Zito
Mwarabu Wa PSG Amtengea Fungu Ronaldo