Tanzania na Afrika ya Kusini kwa pamoja zimedhamiria kuweka mikakati madhubuti ya pamoja ya kujenga na kukuza uchumi wa nchi hizo mbili katika sekta mbalimbali.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Azizi Mlima kwenye ufunguzi wa mkutano wa Tume ya Ushirikiano ya Marais (Bi-National Commission-BNC) Jijini Dar es salaam.

Amesema kuwa wataalamu wa Tanzania na Afrika Kusini wapo katika mkutano wa siku nne wa kuandaa mpango bora wa kushirikiana kwenye maeneo mbalimbali kwa madhumuni ya kukuza uchumi wa nchi hizo.

“Mkutano huu ni muhimu sana kwa kuwa licha ya nchi zetu kuwa na uhusiano na ushirikiano mzuri tokea enzi za ubaguzi wa rangi, lakini bado utakuwa chachu ya kuimarisha na kuharakisha ushirikiano wa kiuchumi na kijamii katika maeneo tutakayokubaliana na wenzetu,” amesema Balozi Mlima.

Aidha, ameongeza kuwa Tanzania na Afrika Kusini zilikubaliana kuanzisha Tume ya Marais ya Uchumi (Presidential Economic Commission-PEC) mwaka 2005 na mwaka 2011 nchi hizo zilisaini BNC ambayo ilichukuwa nafasi ya PEC.

Hata hivyo, Mlima amesema uhusiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Afrika Kusini unaendelea kuimarika kadri siku zinavyokwenda. Kwa takwimu zilizopo takribani makampuni 226 ya Afrika Kusini yamewekeza nchini mtaji wa jumla ya Dola za Marekani milioni 803.15 na kuajiri zaidi ya watu 20,917.

 

Magazeti ya Tanzania leo Mei 9, 2017
"Lionel Messi" nusura aswekwe mahabusu