Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) Mkoa wa Songwe limepewa siku tatu kuandaa mkakati utakaoeleza namna ya kumaliza matatizo ya umeme ikiwemo katizo la mara kwa mara la umeme na tatizo la kiwango kidogo cha umeme.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Mkoa huo, Brig. Jen. (Mst) Nicodemus Mwangela mara baada ya kufika katika ofisi za shirika hilo kufuatia kukatika mara kwa mara kwa umeme na kumtaka Meneja wa shirika hilo kueleza mkakati wa kumaliza tatizo hilo.

Amesema kuwa Mkoa huo unapata athari kubwa kufuatia kutokuwepo umeme wa uhakika kwakuwa shughuli za uzalishaji viwandani, za majumbani zinazohitaji umeme na hata baadhi ya huduma za kijamii zinazohitaji uwepo wa umeme wa uhakika zinaathiriwa huku akielezea kuwa wananchi hawapewi taarifa.

”Nawaelekeza kuanzia sasa mkizima umeme au hata ikitokea hitilafu taarifa na sababu zitolewe ili ifahamike umeme umekatika kwa sababu zipi, tatizo la umeme kwetu limeshakuwa kero kubwa kwani  hakuna maendeleo hususani ya viwanda bila umeme,”amesema Brig. Jen. (Mst) Mwangela.

Aidha, Brig. Jen. (Mst) Mwangela. amewataka TANESCO Songwe waongeze ujuzi na maarifa kutoka kwa maeneo mengine ambao wameweza kutatua matatizo kama hayo pia wafahamu mahitaji ya vifaa vinavyotakiwa kwa ajili ya matengenezo wanayoyafanya.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Songwe, Aristidia Clemence amesema kuwa kukatika umeme mara kwa mara kunatokana na Mvua zonazoendelea kunyesha kwani husababisha nguzo kuanguka na pia radi hupasua vikombe katika nguzo.

Hata hivyo, wananchi Mkoani Songwe wameiomba serikali iwasaidie uwepo wa umeme wa uhakika ili waweze kuzalisha na kufanikisha uchumi wa viwanda.

Video: Tandale yawa Fursa, Biashara kwa Vijana
Kaya zaidi ya 2086 zakumbwa na mafuriko