Klabu ya Simba imeanza kuiwakilisha Tanzania ikiminyana na klabu ya JS Saoura ya Algeria muda huu katika uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Barani Afrika, hatua ya makundi.

Wekundu hao wa Msimbazi ambao wameingia uwanjani wakiwa na kikosi kizima cha maangamizi chenye wachezaji hatari Emmanuel Okwi, John Bocco, Clatous Chama, Hassan Dilunga, James Kotei, Pascal Wawa, Juuko Murdish, Mohammed Hussein, Nicolas Gyan, Jonas Mkude na  mlinda mlango Aishi Manula wanabeba dhamana ya sababu za furaha za Watanzania baada ya dakika 90 leo.

Okwi amekuwa mchezaji wa kwanza wa Simba kuamsha shamrashamra za mashabiki ambao walikuwa wamelala, baada ya kuambaa-ambaa na mpira na kujaribu bahati yake kwa mkwaju ambao hata hivyo uliishia hewani.

Simba wameonesha kuutawala mchezo hadi katikati ya nusu ya kipindi cha kwanza, ambapo Okwi aliweza tena kuwashtua mashabiki wa Simba akipiga mkwaju ambao uligonga mwamba.

Msemaji wa Simba, Hajis Manara amewahakikishia mashabiki kuwa leo wataibuka na ushindi licha ya kuitwa ‘underdog’ kwenye mchezo huo.

Mpira dakika 90, Simba wana mtihani mbele ya JS Saoura ambao wamehamasishwa na nchi yao kuzinyakua alama 3.

Huu ni mchezo mkubwa wa kwanza ndani ya uwanja wa Taifa kwa mwaka 2019, na Simba wana nafasi ya kuandika historia kubwa leo.

Endelea kuitembelea Dar24 tukujuze kama Simba watafanikiwa kuwatafuta Tai wa Algeria au watadonolewa wao.

Aweso azindua mradi wa maji mkoani Kagera
Mwalimu anyweshwa sumu na wasiojulikana