Kutokana na fununu zinazoibuka kila kukicha juu ya kuhitajika kwa beki wa Simba, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ au Zimbwe Jr kwenda timu nyingine, uongozi wa Wekundu hao umeamua kuweka wazi dau la mchezaji huyo kwa timu inayotaka kumnunua.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe ametamka kuwa kulingana na kiwango na mchango alionao mchezaji huyo, thamani yake kwa timu yoyote itakayomtaka kwa sasa ni dola 600,000 (zaidi ya shilingi bilioni 1.3), ambapo kikitolewa kiwango hicho wao wapo tayari kumpa ruhusa kuondoka.

Mchezaji huyo amekuwa akitajwa kuwaniwa na Yanga hivi karibuni, hivyo hiyo ni kama kutangaziwa dau mapema na Wekundu hao kwamba kama wapinzani wao hao watahitaji huduma ya mchezaji huyo lazima watoe kitita hicho na kuweka rekodi ya usajili Bongo kwani haijawahi kutokea.

“Kijana anafanya kazi nzuri kwa sasa, kila mmoja anaiona, tumesikia kuwa kuna klabu zinamtaka na si vizuri kumfuata yeye mwenyewe kwa kuwa bado yupo ndani ya mkataba.

“Sasa kutokana na kiwango na mchango alionao ndani ya timu, kwa klabu yoyote itakayomhitaji, thamani yake ni dola laki sita. Soka limefikia huko kwa sasa.“Miaka ya nyuma ilikuwa dola 80,000, dola laki moja au mbili lakini soka limebadilika sasa na ukiangalia mchezaji kama huyu anayefanya kazi yake sawasawa hilo ndiyo dau lake kwa timu yoyote itakayomtaka kwa ajili ya huduma ya uwanjani,” alisema Poppe.

Tshabalala ambaye alijiunga na timu hiyo msimu wa 2014/15 akitokea Kagera Sugar, amebakiza mwaka mmoja klabuni hapo huku kiwango chake kikizidi kukua kila kukicha akiwa na wastani wa kutoa asisti tatu katika mechi nne walizocheza mpaka sasa msimu huu.

Katika kutambua mchango wa beki huyo wa kushoto anayetajwa kusajiliwa Simba kwa Sh milioni 12 akitokea Kagera, mwanzoni mwa wiki hii, Hans Poppe alimzawadia gari aina ya Toyota Raum ikiwa kama zawadi kwa kazi yake nzuri muda wote akiwa katika kikosi hicho.

Alipoulizwa juu ya suala hilo, beki huyo alisema: “Siwezi kuzungumza suala lolote kuhusu usajili au mkataba wangu, hilo ni suala ambalo lipo kwa meneja wangu, unaweza kuwasiliana naye.”

Alipotafutwa mmoja wa watu wanaomsimamia Tshabalala, Heri Mzozo hakupatikana kwa kuwa simu yake ilikuwa ikiita bila kupokelewa kwa muda mrefu.

Hans van Der Pluijm: Tutachukua Chetu Mapema
Kilimanjaro : Ajiua baada ya kuhukumiwa miaka 60 jela