Serikali imezindua mfumo mpya wa kielektroniki ‘Takukuru App’ utakaotumika kudhibiti askari wa usalama barabarani wanao pokea rushwa.

Uzinduzi wa mfumo huo umefanyika sambamba na uzinduzi wa kampeni ya Utatu yenye lengo la kuongeza mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa barabarani kwa kushirikisha Takukuru, Jeshi la Polisi na wadau mbalimbali.

Mfumo huo wa ‘Takukuru App’ utawezesha wananchi kutuma taarifa za vitendo vya rushwa zinazotokea sehemu mbalimbali nchini kwenda Takukuru.

Mwananchi atakuwa na uwezo wa kupakuwa na kuwa nao mfumo huo kwenye simu yake ya mkononi, utamuwezesha kuonesha eneo ambapo tukio la rushwa linafanyika, kutoa ufafanuzi wa tukio lenyewe ili maofisa wa Takukuru waweze kufuatilia, kisha atatuma ujumbe huo kwenda Takukuru na kupewa mrejesho wa kupokewa kwa ujembe alioutuma.

Faida nyingine ya mfumo huo utaliwezesha Jeshi la Polisi kuona taarifa hizo na kufanya uchunguzi kisha kutoa mrejesho wa hatua zilizochukuliwa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala  Bora, George Mkuchika, amewataka wananchi kutoa taarifa za ukweli kupitia App hiyo bila kuwaonea watu ambao wana visa nao kwa mambo binafsi.

Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro, amesema matumizi ya Teknolijia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) yatasaidia kupunguza vitendo vya rushwa barabarani.

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Novemba 3, 2019
Wanajeshi 35 wauawa kwenye shambulio Mali