Baada ya kuifunga Congo-Brazzaville mabao 3-2 katika mchezo wa kwanza kuwania nafasi ya kucheza Kombe la Mataifa ya Afrika, timu ya taifa Serengeti inatarajiwa kuondoka Alhamisi wiki hii kwenda kupiga kambi nje ya mipaka ya Tanzania.

Hata hivyo, taratibu zinapangwa kuhakikisha kwamba timu hiyo inakwenda kupiga kambi kwenye nchi tulivu inayolingana hali ya hewa na Congo Brazzaville kadhalika chakula pamoja na mazingira. Tanzania na Congo Brazzavile, zinatarajiwa kurudiana Oktoba 2, 2016 huko Congo Brazzaville na timu itakayopata ushindi wa jumla katika michezo miwili itafuzu kwa fainali hizo.

Katika mchezo uliofanyika jana Septemba 18, 2016 timu hiyo ya Tanzania maarufu kwa jina la Serengeti Boys ilipata mabao yake kupitia Yohana Mkomola na Abdi Makamba wakati yale ya Congo yalifungwa na Langa-Lesse Percy na Makouana Beni ambao mashabiki wa soka walikuwa wakiwalalamikia kuwa ni “wakubwa.”

Ili ifuzu kwa fainali zitakazofanyika mwakani huko Antananarivo, Madagascar katika fainali zitakazoanzia Aprili, 2017, Serengeti Boys inatakiwa ibaki na matokeo yake ya sasa na ihakikishe inapata ushindi na kama sare basi wapate bao kufuta faida ya bao la ugenini ambalo Congo Brazzaville walikuwa wanasheherekea  baada ya mchezo.

Diamond Trust Bank Yadhamini Ligi Kuu Tanzania Bara
African Lyon Kuwakaribisha Toto Africans Uwanja Wa Uhuru