Mshambuliaji wa Klabu ya Juventus, Cristiano Ronaldo ameandika historia mpya akimfunika mpinzani wake kwenye mbio za uchezaji bora na upachikaji magoli, Lionel Messi baada ya kupachika goli la 600 jana walipokutana na Inter Milan.

Ronaldo alipachika goli hilo la 600 katika maisha yake ya kutumikia Klabu, akiisawazishia timu yake katika dakika ya 62 ya mchezo baada ya kupigwa na Radja Nainggolan katika dakika ya 7 ya mchezo huo wa Serie A.

Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 34 amejiweka mbele ya Messi ambaye ameifungia Barcelona magoli 597.

Hata hivyo, tofauti na Messi ambaye amekuwa na klabu moja, Ronaldo amefikisha idadi hiyo ya magoli akiyakusanya wakati anatumikia klabu za Sporting CP, Manchester United, Real Madrid na sasa Juventus.

Ingawa Juventus wamepata pigo kwenye Ligi ya Mabingwa, hususan kwenye mchezo wa robo fainali dhidi ya Ajax, usajili wa Ronaldo ulioigharimu timu kiasi kikubwa cha fedha umekuwa na matokeo makubwa chanya ndani ya klabu hiyo kwenye msimu huu.

Aidha, Ronaldo pia anamiliki magoli 85 aliyoifungia timu yake ya Taifa ya Ureno, ikiwa ni pamoja na hat-tricks, inayokumbukwa zaidi ni ya Kombe la Dunia dhidi ya Morocco nchini Urusi, katika Fainali zilizofanyika Juni mwaka jana.

Klabu hiyo inaongoza Ligi hiyo ya Italia ikiwa na alama 88, ikifuatiwa kwa mbali na Napoli 67.

 

Akothee anunua ugomvi wa Mange na Zari, ampasua Mange
Picha: Idris Elba afunga ndoa na Sabrina