Tanzania imetajwa kuwa nchi inayoongoza kwa kuwa na watumiaji wengi wa madawa ya kulevya aina ya bangi katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa mujibu wa ripoti ya utafiti iliyotolewa na shirika la New Frontier, kati ya waliopitiwa na utafiti huo, Watanzania milioni 3.6 walikiri kuwa wanatumia bangi.

Utafiti huo uliochapishwa kwenye gazeti la The Citizen, Mei 27, 2019 unaitaja Tanzania kuwa nchi ya tano barani Afrika kwa kuwa na idadi kubwa zaidi ya watumiaji wa bangi.

Kwa Afrika Mashariki, Kenya inashika nafasi ya pili ikiwa na watumiaji milioni 3.3 huku ikishika nafasi ya sita barani Afrika na Uganda inafuata ikiwa na watumiaji milioni 2.6 na inashika nafasi ya nane Afrika.

Utafiti huo unaitaja Nigeria kuwa ndiyo yenye watumiaji wengi zaidi wa bangi barani Afrika, ambapo watu milioni 20.8 wanavuta. Ethiopita imetajwa kuwa na watumiaji milioni 7.1 ikishika nafasi ya pili, Misri wapo milioni 5.6 inashika nafasi ya tatu, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) watumiaji milioni 5 ikishika nafasi ya nne.

Uvutaji wa bangi ni kosa la jinai katika nchi hizi na zao hilo ni moja kati ya mazao yanayotajwa kwenye orodha ya madawa ya kulevya ambapo adhabu yake huwa kubwa.

Kwa mujibu wa utafiti huo, duniani kote, watu milioni 260 wamebainika kuwa hutumia bangi angalau mara moja kwa mwaka na kwamba dola bilioni 344 ($344 bilioni) hutumika kila mwaka kununua bangi.

Video: Nyalandu akamatwa, Sakata la makinikia lafufuliwa bungeni
LIVE: Yanayojiri Bungeni jijini Dodoma Mei 28, 2019