Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Felix Tshisekedi amesema kuwa tayari ameshaomba kujiunga na nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ameyasema hayo Jijini Dar es salaam mara baada ya kufanya ziara fupi katika bandari ya Dar es salaam katika ziara yake ya siku mbili hapa nchini Tanzania.

Amesema kuwa ziara hiyo ina lengo la kuimarisha mahusiano na kujenga misingi imara ya kiuchumi na biashara baina ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

”Katika ziara hii hapa Tanzania, kuna mengi nimejifunza, kikubwa tunalenga kuimarisha miundombinu ili iweze kurahisisha suala zima la maendeleo hasa usafirishaji ambao utasaidia sana katika sekta ya biashara na uchumi,”amesema Tshisekedi

Aidha, katika hatua nyingine, Tshisekedi amesema kuwa tayari nchi yake imeshaomba kujiunga na Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki.

Vile vile amesema kuwa ili kuweza kufikia malengo hayo waliyojiwekea ya kibiashara, ni lazima kuwepo na ushirikiano wa hali ya juu hasa katika ujenzi wa miundombinu ambayo itarahisisha zaidi kuleta maendeleo na kukuza uchumi wa nchi husika.

Hata hivyo, ameongeza kuwa amejifunza mengi na yapo mengi ya kujifunza kwa viongozi wa Tanzania, hasa kwa Rais Dkt. John Magufuli katika suala zima la namna ya kukuza uchumi.

 

Hakuna mtu atakayekamatwa kwa kukutwa na vifungashio- Makamba
Kabla ya Bajeti kusomwa Kenya, Wabunge wanawake walisusia kikao