Rais wa Urusi, Vladimir Putin ametahadharisha kuwa hakuna atakasalia kama itatokea vita kamili ya mgogoro wa kinyuklia kati ya nchi hiyo na Marekani.

Putin ameyasema hayo katika mahojiano na muongozaji wa filamu wa Marekani, Oliver Stone alipotaka kupata mtazamo wake kuhusu mgogoro kati ya mataifa hayo makubwa na yenye nguvu.

Aidha, Rais huyo wa Urusi alipoulizwa kama kuna matumaini yoyote ya kumalizika kwa mgogoro huo alijibu, “kuna matumaini siku zote. Hadi watakapokuwa tayari kutupeleka makaburini na kutuzika.”

Katika hatua nyingine, Putin aliukosoa muungano wa NATO akidai kuwa ni chombo kinachotumiwa kutekeleza sera za nje za Marekani.

“Punde tu nchi inapojiunga na muunganowa NATO, ni vigumu kukataa msukumo kutoka Marekani na kwa bahati mbaya mfumo wowote wa silaha za Marekani unaweza kuwekwa ndani ya nchi hiyo, ikiwa ni pamoja na kuwekwa makazi mapya ya vikosi vya Marekani,” alisema Putin.

Alisema kutokana na hali hiyo, Urusi inaendelea kuchukua hatua za kujihami dhidi ya NATO na kuunda ngao za kijeshi katika mipaka yake.

Katika hatua nyingine, Putin alijibu swali la Stone aliyetaka kupata maelezo yake baada ya kumueleza kuwa ana taarifa za kutosha kuwa rais huyo ameshanusurika katika majaribio makubwa matano ya kumuua.

“Ninafanya kazi yangu na maafisa usalama pia wanafanya kazi yao, na hadi sasa wanafanya kazi yenye mafanikio sana,” alijibu.

Marekani na Urusi wamekuwa katika mgogoro wa muda mrefu, na sasa hali ilianza kuonekana kutulia baada ya Donald Trump anayedaiwa kuwa rafiki wa Putin kuchaguliwa kuwa Rais wa Marekani.

Video: Mghwira apinga ACT, Ni Bonge la Bajeti
Al-Shabab wavamia kambi ya jeshi la Somalia