Jopo la majaji wa Chicago limepitisha mashtaka 16 yaliyofunguliwa na Polisi dhidi ya muigizaji wa Series ‘Empire’, Jussie Smollett maarufu kama Jamal baada ya kumtuhumu kuwa alidanganya kuhusu kufanyiwa shambulizi la unyanyasaji na ubaguzi.

Waendesha mashtaka wameeleza kuwa muigizaji huyo mwenye umri wa miaka 36 mwenye asili ya Afrika, aliwalipa rafiki zake wawili raia wa Nigeria kutengeneza tukio la kihalifu dhidi yake baada ya kutoridhishwa na mshahara anaolipwa.

Uchunguzi wa tukio hilo umeonesha kuwa Smollett alinunua mwenyewe vifaa vilivyotumika katika tukio hilo, ikiwa ni pamoja na kamba waliyomfunga.

Smollet aliripoti polisi akidai kuwa alivamiwa alipokuwa anaenda kutafuta chakula usiku wa manani, akipita katika mitaa ya Chicago. Alidai waliomshambulia walitamka maneno yanayoashiria kuwa ni wafuasi wa Rais Donald Trump.

Hata hivyo, uchunguzi wa awali wa polisi kupitia kamera za CCTV pamoja na kuwahoji wanaume wawili walioonekana wakimshambulia, ulibaini kuwa alipanga kila hatua na aliwalipa watu hao.

Jana, msemaji wa Idara ya Polisi ya Chicago, Anthony Guglielmi alisema kuwa kitendo alichokifanya ni cha aibu na kinawaaibisha majirani zake ambao waliishi naye vizuri na kumheshimu kama msanii anayewahamasisha.

“Kitendo alichokifanya Bw. Smollet ni cha aibu na kama itathibitika hivyo, itakuwa amewaaibisha watu wa Chicago ambao walimpenda na kumtunza kama jirani na mtu anayewahamasisha. Sisi tuko nyuma ya kazi ya wapelelezi,” alisema.

Empire walitangaza kumfuta kazi mara moja muigizaji huyo ambaye alikuwa miongoni mwa wahusika wakuu, akiigiza kama mtu anayejihusisha na mapenzi ya jinsia moja na mwenye kipaji cha kuimba cha hali ya juu.

Video: JK aongoza maelfu kuaga mwili wa Kibonde jijini Dar
Dkt. Raphael Chegeni awashika mkono Wanawake na Vijana Busega