Jeshi la Polisi mkoa wa Singida linamshikilia mbunge wa Manyoni, Daniel Mtuka (CCM) kwa tuhuma za kumuua mwanafunzi wa darasa la kwanza kwa kumgonga na gari alipokuwa akijaribu kuvuka barabara mkoani hapo.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoa wa Singida, Debora Magilingimba, Mbunge huyo (pichani) aliyekuwa akisafiri na gari lake aina ya Toyota Prado alimgonga mwanafunzi huyo na kwamba uchunguzi wa awali unaonesha kuwa chanzo cha ajali ni uzembe wake wa kutochukua tahadhari kwa watumiaji wengine wa barabara.

Kamanda Magilingimba alisema kuwa jeshi hilo linamshikilia Mtuka tangu jana kutokana na tukio hilo na watamfikisha mahakamani kwa ajili ya hatua za kisheria.

“Mtuhumiwa Mtuka anashikiliwa na jeshi la polisi kwa mahojiano na baada ya mahojiano, atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma inayomkabili,” alisema Kamanda Magilingimba.

Aliongeza kuwa mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya wilaya ya Manyoni kwa uchunguzi wa madaktari.

Mbowe: Kilimanjaro hatutegemei CCM kuleta maendeleo
Raila ahudhuria utangazaji wa matokeo akiwa na kitendawili