Wakati dunia ya masumbwi ikisubiri kwa hamu tangazo la pambano la marudiano kati ya wababe Manny Pacquiao na Floyd Mayweather, imethibitishwa kuwa wawili hao watapambana hivi karibuni kwenye aina nyingine ya mchezo nchini Ufilipino.

Mayweather ambaye anafanya ziara yake nchini Ufilipino, amethibitisha kuwa ataingia katika uwanja wa mpira wa kikapu na kucheza dhidi ya Pacquiao nchini humo.

Akizungumza wakati wa kumtangaza Mayweather kuwa balozi wa Belo Medical Group, Dkt. Victoria Belo ameeleza kuwa, “ atacheza mpira wa kikapu dhidi ya Pacquiao leo.” Mayweather alionesha kukubali kwa kutikisa kichwa na kisha kukazia kwa kutaja jina la eneo watakalokutana kwenye mchezo huo.

“Nimezunguka dunia wakati wote na nimekuja Ufilipino tena, na nimevutiwa na watu wa nchi hii, eneo zuri, watu wazuri wako chanya sana,” alisema Mayweather.

Katika hatua nyingine, bondia huyo alizungumza na FightHype na kukanusha taarifa kuwa wamefikia makubaliano ya kupambana tena na Pacquiao.

Mayweather na Pacquiao walipigana miaka minne iliyopita katika pambano ambalo liliandika historia ya kuwa pambano lililoingiza fedha nyingi zaidi katika historia. Mayweather alishinda kwa mbali, ingawa pambano hilo liliacha mjadala mkubwa wa utata wa matokeo, licha ya matokeo ya majaji wote watatu kumpa Mayweather ushindi wa nguvu.

Mwaka jana, Mayweather ambaye hajawahi kupoteza pambano kati ya mapambano 50, alikutana na Pacquiao nchini Japan ambapo walionekana kuzungumza na kutambiana, kisha Mayweather ambaye amestaafu masumbwi akatangaza kuwa atarejea tena ulingoni kwa ajili ya pambano la la marudiano.

50 Cent auza jumba lake la kifahari na kugawa fedha zote kama msaada
Pierre aeleza wanachokosea wanywaji hadi kuamka na ‘hangover’