Aliyekuwa Rais wa Sudan, Omar al-Bashir amekamatwa usiku wa Jumanne na kupelekwa gerezani baada ya kupinduliwa madarakani katika mapinduzi ya kijeshi jijini Khartoum.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka shirika la habari la kimataifa la Reuters, kiongozi huyo mwenye miaka 75 ambaye ameiongoza nchi hiyo kwa miaka 30 amekamatwa na kupelekwa kwenye gereza lenye ulinzi mkali la Kobar mjini Khartoum.

Kiongozi huyo alikuwa chini ya ulinzi mkali wa jeshi nyumbani kwake toka alipopinduliwa, ambapo sasa anashikiliwa kwenye chumba cha peke yake gerezani na kuzungukwa na ulinzi mkali.

Nchi ya Sudan ipo chini ya uongozi wa Baraza la Mpito la Kijeshi chini ya Luteni Jenerali Abdel Fattah Abdelrahman Burhan, katika hotuba yake kwenye televisheni kuung’oa utawala, na kuahidi kuheshimu haki za binaadamu, kusitisha marufuku ya kutotoka nje, kuwaachia huru wafungwa wa kisiasa, kuvunjilia mbali serikali zote za majimbo, kuwashtaki waliowaua waandamanaji na kukabiliana na rushwa.

Aidha, wananchi wamekuwa wakiandamana kulishinikiza jeshi kuachia madaraka kwa uongozi wa kiraia, ambapo msemaji wa baraza Meja Jenerali Shams Ad-din Shanto ameeleza kwamba baraza la kijeshi lipo tayari kuidhinisha Serikali yoyote ya kiraia itakayoidhinishwa na vyama vya upinzani.

CUF waeleza walivyopania kuchukua ubunge wa Zitto
Chanzo cha moto Kanisa kuu la Notre Dame chatajwa, Rais aahidi kulijenga uypya