Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha ameitaka Serikali ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara kuhakikisha inahusisha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA katika ujenzi wa Chuo cha VETA Simanjiro ili miundombinu ya chuo hicho iweze kujengwa kwa utaratibu na viwango vinavyohitajika.

Ametoa agizo hilo Mkoani Manyara wakati akikagua eneo ambalo Serikali ya Wilaya hiyo inategemea kujenga Chuo cha Veta kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Hiari ECLAT.

Amesema kuwa ni vizuri Mamlaka husika zikahusishwa katika ujenzi wa Chuo hicho tangu hatua za awali na kumtaka Mkurugenzi wa VETA kanda  na yule wa Mkoa kufika katika eneo la Emboreet ambako mradi utajengwa kwa lengo la kuongea na wananchi pamoja na wafadhili wa mradi huo ili wazo ambalo limeanza liweze kutekelezwa kwa utaratibu unaostahili.

“Ninyi Halmashauri mnataka kujenga chuo cha Ufundi ni wazo zuri lakini ni lazima kijengwe kwa utaratibu sio kiholela kwa sababu vilianza kuibuka vyuo ambavyo mtu anakuwa na jengo moja anasajili kinaitwa chuo, kuna viwango na masharti ambayo ni lazima yatimizwe kabla chuo kuruhusiwa kufanya kazi, fuateni taratibu hizo ili muweze kuanzisha chuo cha Ufundi,” amesema Ole Nasha.

Aidha, amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imeweka mkazo mkubwa katika Elimu ya Ufundi kwa kuwa kuna vijana wengi wanaomaliza shule wanaishia kutokuwa na ajira kwa kuwa hawana maarifa yanayowasaidia kupata ajira hasa pale wanapokosa fursa ya kuendelea na elimu ya juu hivyo ujenzi wa vyuo vya ufundi vingi utasaidia kuwajengea vijana wengi uwezo wa kujiajiri

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Yefred Myenzi amesema kuwa wazo la kuanzisha Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi katika Wilaya hiyo ni kuwawezesha vijana kuweza kupata maarifa ya kuweza kujiajiri badala ya kusubiri kuajiriwa.

Naye Meneja Mradi ya ECLAT Bakiri Angalia amesema pamoja na shirika hilo kushiriki ujenzi wa Chuo hicho lakini pia katika Wilaya hiyo imefadhili miradi ya Elimu yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 3.

 

Jaji Mkuu awafunda viongozi wa Mahakama
Video: Serikali haitamvumilia kiongozi atakayekiuka maadili - Waziri Mkuu