Mamlaka ya vitambulisho vya Taifa (NIDA), imefunga mitambo miwili yenye uwezo wa kuzalisha vitambulisho 9,000 kwa saa ikiwa na uwezo mkubwa zaidi kulinganisha na mitambo iliyokuwepo awali iliyokuwa inazalisha vitambulisho 200 – 250 kwa saa.

Taarifa  hiyo imetolewa na kitengo cha mawasiliano na uhifadhi hati NIDA kwa nia ya kufafanua taarifa ya uongo kuwa uwezo wa NIDA kwa sasa ni kuzalisha vitambulisho 1,000 tu kwa siku na kudaiwa kuwa watalazimika kuchukua miaka 82 kuzalisha vitambulisho milioni 51.1.

NIDA imefafanua kuwa vitambulisho milioni 15 vinaweza kuzalishwa kwa kipindi cha miezi mitatu tu kwa kutumia mitambo yake hiyo.

Aidha taarifa hiyo imefafanua kuwa, imewasiliana na mamlaka mbalimbali za Serikali kwaajili ya hatua zaidi na kuanza utozaji  tozo na inatambua kuwa kutokana na umuhimu wa mfumo huo, serikali imewekeza kiasi kikubwa cha fedha ili taasisi, wafanyabiashara na wananchi waweze kutumia taarifa za utambulisho kwa shughuli za kijamii.

Hivyo imeelezwa kuwa utozaji wa tozo ni moja ya namna ya kurudisha gharama za uwekezaji uliofanywa na Serikali na pia kuwa na mfumo wa utambuzi endelevu.

Kabendera aachiwa huru, apunguza faini milioni 100
Kigwangalla aridhishwa matengenezo barabara Ngorongoro