Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai ametoa onyo kali kwa waandishi wa habari waliopo bungeni ambao wanaripoti  habari za Bunge na kuwahoji wabunge wanaotoka ndani ya ukumbi wa Bunge na kususia vikao vya bunge.

Ambapo Ndugai amepiga marufuku kwa waandishi hao kufanya mahojiano na wabunge wanaosusia vikao vya bunge na kwa yeyote atakaye kiuka agizo hilo amesema atanyang’anywa kitambulisho na kuondolewa bungeni na hatoruhisiwa kuripoti habari za bunge.

”Hawa wabunge wanaosusa vikao huku ndani wakitoka nje waandishi wanawakimbilia kuwahoji. Sasa napiga marufuku Mwandishi yeyote atakayeonekana nje ya ukumbi wa Bunge anamhoji mbunge aliyesusa kikao, atanyang’anywa kitambulisho na hataruhusiwa kuripoti habari za bunge wala hatakanyaga tena hapa” amesema Job Ndugai.

Hayo yamesemwa leo April 4, 2019 ambapo kumezuka tabia ya wabunge wa upinzani kususia vikao vya bunge.

Tabia hii imezuka katika kikao kilichofanywa tarehe 3 na tarehe 4, April 2019 mara baada ya kamati ya maadili kuwawajibisha wabunge wawili wa chama cha Upinzani Chadema, Mbunge wa Kawe Halima Mdee na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema ambao mbele ya kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge wameshindwa kuthibitisha kauli zao zilizodai kuwa Bunge ni dhaifu.

Ambapo wabunge hao wamesimamishwa kuhudhuria mikutano ya bunge kwa kipindi fulani kama namna ya kutumikia adhabu yao, hivyo maazimio hayo yamewafanya wabunge wengine wa upinzani kususia vikao viwili vya wabunge.

Hivyo Job Ndugai amewatahadharisha waandishi wa habari wanaowakimbilia wabunge hao na kuwahoji na kupiga marufuku mwandishi yeyote kuchukua taarifa kutoka kwa wabunge hao.

Mputu aitishia Simba, 'Tunajua hawafungiki nyumbani'
Msimamo wa Lema, ''Sitanyamaza hata kama adhabu itakuwa mauti’’