Mwenyekiti wa baraza la wazee wa Yanga, Ibrahim Akilimali amesema kuwa iwapo angekuwa mzima wa afya angefanya maandamano hadi kwa Waziri Mkuu, Kasim Majaliwa kushinikiza viongozi wa klabu hiyo waachie madaraka.

Mzee Akilimali amesema kuwa anashangazwa na aina ya uongozi wa Yanga chini ya mwenyekiti, Mshindo Msolla ambapo kuna baadhi ya mambo yanafanywa si sahihi likiwemo suala la kumpa timu kocha Charles Boniface Mkwasa kwa kuwa hana jipya.

“Uongozi wetu unafanya mambo ya ajabu sana, mambo mengi ambayo wanayafanya ni kinyume, ona sasa tumeruka kihunzi tumekanyaga matope, yaani tumemuondoa Zahera wanatuwekea Mkwasa, sasa wa kazi gani na wakati hana jipya la kufanya.

“Alikuwepo pale Yanga alifanya nini, alipewa timu ya taifa ya vijana alifeli, alipewa timu ya akina mama hakuna alichokifanya na hata timu ya taifa ya wakubwa, zote hizo hakufanya kitu chochote na badala yake aliondolewa kote huko, sasa nashangaa kwa nini viongozi wetu wamempatia majukumu hayo.

“Huu uongozi siutaki hata kidogo haufai, kwa sasa mimi ni mgonjwa, nigekuwa siumwi ningefanya maandamano hadi kwa waziri mkuu ili kuweza kuupinga uongozi huu uondoke madarakani.

“Pia ili mambo yaweze kwenda sawa ndani ya klabu ni lazima kuwe na ushirikiano wa sisi wenyewe ili kuweza kutoa maamuzi ya pamoja linapokuja jambo la kimaslahi ndani ya timu kuliko watu kutofautiana pindi maamuzi yanapofanyika kwa upande mmoja.” alisema Akilimali.

Uongozi mpya wa Yanga uliingia madarakani tangu Mei, mwaka huu baada ya klabu hiyo kukaa kwa muda mrefu bila ya viongozi kufuatia aliyekuwa mwenyekiti wa klabu hiyo, Yusuph Manji kujiengua.

kitunguu maji ni dawa
Miriam Odemba mwanamitindo aliyeokoka