Mbunge wa Iramba Magharibi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mwigulu Nchemba amesema kuwa ajali aliyoipata imesababishwa na Punda waliokuwa wakikatisha barabarani.

Ameyasema hayo katika hospitali ya Mkapa jijini Dodoma anakopatiwa matibabu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambapo amesema kuwa alikuwa akitokea mkoani Iringa kuelekea mkoani Singida kuhudhuria kikao cha kamati ya siasa.

“Nilikuwa siangalii mbele kwa kuwa nilikuwa naongea na simu lakini ghafla nilishtushwa na tahadhari ya ajali niliyopewa na dareva wangu, nilipotazama mbele niliwaona punda watatu wanakatisha barabara na mmoja alifanikiwa kuvuka na kuwagonga wengine wawili. Nilichosikia ni sauti ya kishindo kikubwa kilichoashiria kuwa tumepata ajali, namshukuru Mungu ni mwema kwa kuwa ametuepusha na kifo,” Amesema Mwigulu

Aidha, amesema kuwa baada ya hapo aliona moshi umetanda ndani ya gari hali iliyoashiria gari hilo lingeweza kulipuka lakini wasamalia wema walifika na kuwaokoa na kuwawahisha hospitali ya Benjamin Mkapa.

Hata hivyo, mapema asubuhi ya leo taarifa za Mwigulu Nchemba kupata ajali zilisambaa huku chanzo kikiwa hakijatajwa mpaka pale alipozungumza mwenyewe.

Dkt. Hawasi apokea wanachama wapya zaidi ya 115
Mwanaharakati aliyetoweka akutwa amefariki dunia