Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Kenya imepinga vikali mahakamani maombi yaliyowasilishwa mahakamani ya kutaka kuhalalishwa kwa mapenzi ya jinsia moja.

Muwasilisha maombi amejaribu kuishawishi mahakama hiyo kuwa mapenzi ni tendo la faragha ambalo ni haki ya kikatiba ya kila mwananchi, hivyo kama haitamaanisha kufunga ndoa ihalalishwe.

Akiwakilisha Ofisi hiyo, mwanasheria Jennifer Gitiri aliiambia mahakama kuwa kuhalalisha vitendo hivyo vitasababisha kuvunjwa kwa maadili, na kwamba itapelekea watu hao kufunga ndoa na kuvunja Ibara ya 45 ya Katiba inayotambua ndoa kuwa ni kati ya mume na mke.

“Kama ndoa ni kati ya mwanaume na mwanamke, kwanini vitendo viovu kati ya watu wa jinsi moja vihalalishwe? Hii inaonesha wazi kuwa baadaye watafikia hatua ya kufunga ndoa ambayo ni kinyume cha katiba,” alisema.

Awali, mleta maombi, mkurugenzi wa tume ya haki za mashoga, Eric Gitari aliomba mahakama kutangaza kifungu cha 162 na 165 vya Kanuni ya Adhabu (Penal Code) kuwa kinyume cha katiba. vifungu hivyo vinatoa adhabu kali kwa mtu anayejihusisha na mapenzi ya jinsia moja au kujihusisha kimapenzi na mnyama.

Kesi hiyo bado inaendelea na mchakato wa kimahakama.

NEC yakikaba koo kituo cha sheria LHRC
Video: Wiki ya majonzi, Kigogo Chadema auawa kinyama