Jeshi la polisi mkoa wa Njombe limefanikiwa kumpata mtoto wa miezi mitano aliyetelekezwa nyumba ya kulala wageni na kumuhifadhi chini ya uangalizi wa idara ya ustawi wa jamii.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Njombe, Hamis Issa ametoa taarifa hiyo kwa wanahabari mkoani humo akibainisha kuwa mtoto huyo amekutwa kwenye nyumba ya kulala wageni inayofahamika kama Shamba Guest House iliyopo mjini Njombe huku akiachiwa ujumbe.

“Shamba Guest amekutwa mtoto ambaye ana umri mdogo zaidi na ametelekezwa na mwanamke ambaye ni mama yake na ameacha ujumbe amesema anaenda eneo la Mwanza na huyu msaidizi amemuachia huyo mtoto,na pindi mambo yatakapo kuwa mazuri atamtumia hela” amesema kamanda Issa.

Kwa mujibu wa kamanda mwanamke huyo anafahamika kwa jina la Stella Mtweve na mtoto huyo wa kiume mwenye umri wa miezi mitano na nusu  ametambuliwa kwa jina la Kelvin Mmagoma .

Lugola awaonya wanaosafirisha wahamiaji haramu
Mahakama yaamuru Wabunge wa Chadema wenye kesi ya uchochezi wakamatwe