Misri imeutuhumu Umoja wa Mataifa kwa kutaka kuingiza siasa katika kifo cha rais wa zamani wa nchi hiyo, Mohamed Morsi mara baada ya kuitisha uchunguzi huru.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Misri, Ahmed Hafez amesema kuwa amelaani vikali wito wa msemaji wa Tume ya Haki za Binaadamu ya Umoja wa Mataifa, Rupert Colville, wa kufanywa uchunguzi huru kuhusu kifo cha Morsi kilichotokea Jumatatu wakati wa kikao cha kusikilizwa kesi yake mahakamani.

Hafez amesema kuwa ni jaribio la makusudi la kuingiza siasa katika kifo cha kawaida cha rais wa zamani wa nchi hiyo kilichotokea siku ya Jumatatu.

Colville ametoa wito wa kufanywa kwa uchunguzi huru ili kuweza kubaini kama mazingira ambayo Morsi alikabiliana nayo kwa kipindi cha miaka sita akiwa kizuizini kama yalichangia kifo chake.

Hata hivyo, Morsi aliondolewa madarakani na aliyekuwa wakati huo mkuu wa jeshi na sasa Rais wa nchi hiyo, Abdel Fattah al-Sissi baada ya kukaa mwaka mmoja pekee madarakani.

Serikali kubuni njia mbadala ya kutibu ugonjwa wa Dengue
Fahamu undani wa ugonjwa wa siko seli