Shirikisho la soka barani Afrika CAF limemteua Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania TFF Ahmed Mgoyi kuwa Kamishna wa mchezo wa Kombe la Shirikisho kwa klabu kati ya AFC Leopards ya Kenya na Fosa Juniors ya Madagascar.

Mchezo huo namba 13 utachezwa nchini Kenya kati ya Februari 9,10 na 11 mwaka huu.

Kwenye mchezo huo waamuzi wote wanatoka nchini Somalia ambapo mwamuzi wa kati ni Abdulkadir Artan Omar,mwamuzi msaidizi namba moja Ali Mohamed Mahad,mwamuzi msaidizi namba mbili Ahmed Abdullah Farah wakati mwamuzi wa akiba ni Hassan Mohamed Hagi.

Mgoyi ni miongoni mwa Wajumbe wa Kamati ya utendaji wa TFF walioteuliwa hivi karibuni kuwa makamishna wa mechi zinazoandaliwa na CAF kwa mwaka 2018 mpaka mwaka 2020 wengine ni Makamu wa Rais wa TFF Michael Wambura,Amina Karuma na Sarah Tchao.

Aidha Rais wa TFF Ndugu Wallace Karia naye mbali ya kuteuliwa kwenye kamati ya mashindano ya fainali za Africa kwa wachezaji wanaocheza ndani CHAN tayari amechaguliwa mara mbili kusimamia mechi za CHAN zinazoendelea nchini Morocco.

Alisimamia mechi ya ufunguzi iliyowakutanisha Wenyeji Morocco na Mauritania Januari 13, 2018 na mchezo wa pili uliochezwa jana Januari 22, 2018 kati ya Namibia na Zambia.

TFF yakataa viwanja vitatu kombe la shirikisho
Ligi ya wanawake ya Serengeti Premier Lite kuendelea Februari