Mfanyakazi wa shirika la ndege la Alaska ameripotiwa kuiba ndege katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Settle Tacoma uliopo nchini Marekani na kuirusha takribani saa moja kabla ya kuanguka.

Ndege hiyo imetajwa kuwa ni aina ya Bombardie Q400 na ilikuwa imetoka kufanyiwa matengenezo madogo ikisubiri kuanza safari zake saa chache baadaye.

Jeshi la polisi limeeleza kuwa mfanyakazi huyo alikuwa akifanya kazi ya kuongoza ndege zinapotua aliingia ghafla ndani ya ndege hiyo yenye uwezo wa kubeba watu 76, Ijumaa majira ya saa mbili usiku na kuanza kuiendesha hadi umbali wa maili 40.

Mkuu wa Polisi wa eneo la Pierce, Paul Pastor alimtaja mfanyakazi huyo kuwa ni kijana mwenye umri wa miaka 29 ambaye aliiangusha ndege hiyo na kupoteza maisha.

Alisema kuwa baada ya kurusha ndege hiyo ghafla, ndege mbili za kijeshi zilianza kumfuatilia na baadaye ndege hiyo ilimshinda na kuanguka maeneo ya mbali pasipo na makazi ya watu. Ndege zilizomfuatilia zilikuwa salama na hakuna mtu aliyeathirika na ajali hiyo, kwa mujibu wa taarifa hiyo.

“Mioyo yetu iko pamoja na familia za mfanyakazi huyo pamoja na wafanyakazi wetu wote wa mashirika ya ndege ya Alaska & Horizon,” alisema Constance von Muehlen ambaye ni afisa mwandamizi wa oparesheni wa shirika hilo la ndege.

Vyombo vya usalama vimesema kuwa tukio hilo halihusiani na tukio lolote la kigaidi ingawa uchunguzi zaidi unaendelea.

Mashuhuda wa tukio hilo wameeleza kuwa awali walidhani ndege hizo zilikuwa zinafanya mazoezi ya kijeshi.

Trump aiwekea Zimbabwe ‘kisiki’ kingine kisa uchaguzi
CCM yaifunika Chadema udiwani Turwa, Tarime