Mpiganaji wa mapambano ya ngumi na mateke yanayofahamika kama Mixed Martial Art (MMA), Conor McGregor amewashtua wadau wa mchezo huo baada ya kutangaza ghafla kustaafu rasmi.

Tangazo hilo la McGregor limewashtua wadau kutokana na kutokuwepo kwa dalili zozote za awali za kuchukua uamuzi huo huku mashabiki wakisubiri kwa hamu kusikia nani atakayepambana naye siku za hivi karibuni.

“Jamani, nina tangazo la haraka, nimeamua kustaafu rasmi mchezo unaofahamika kama ‘Mixed Martial Art’ leo,” tafsiri ya tweet ya MacGregor, Machi 26.

“Ninawatakia wenzangu kila la kheri wanapoendelea na mashindano. Ninajiunga na washirika wangu wa zamani kwenye hii hatua, tayari nimeanza kuwa mstaafu,” aliongeza mpiganaji huyo mwenye umri wa miaka 30.

Mpiganaji huyo raia wa Ireland mwenye rekodi nzuri ya kushinda mapambano 21 na kupoteza mapambano manne, amechukua hatua hiyo ikiwa ni miezi kadhaa tangu alipopigwa na raia wa Urusi, Khabib Nurmagomedov.

McGregor ndiye mpiganaji pekee wa MMA aliyejitokeza kupigana na mbabe wa masumbwi, Floyd Mayweather lakini alizidiwa ujuzi na kupoteza pambano katika raundi ya 10.

Justin Bieber asitisha kufanya muziki, asimulia yanayomsibu...
Wa kwanza Timu Maalim Seif apewa uongozi ACT-Wazalendo