Khalifa Mohamed Kinyaka (51), anashikiliwa na jeshi la Polisi Mkoani Dodoma, kwa tuhuma za kutorosha na kusafirisha viroba sita vya madini vyenye uzito wa kilogramu 410.75.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoani Dodoma, Gilles Muroto, amesema Kinyaka alikamtwa katika basi la abiria la Jambo Express, lenye namba za usajili T 704 DLF, linalofanya safari zake kati ya Katesh na Dar es salaam.

“Tumemkamata mtuhumiwa huyu mkazi wa Chamwino Mkoani hapa katika basi akiwa na kiroba kimoja cha madini mara baada ya kufanya upekuzi.” Amefafanua Kamanda Muroto.

Amesema mbinu iliyotumiwa na mtuhumiwa ni kupanda basi tofauti na lile alilopakia viroba vingine vitano, katika basi la Emigrace lenye namba za usajili T 730 DGL lililokuwa likiendeshwa na Adrian John Temba (32), likitokea Babati Manyara kuelekea jijini Dar es salaam.

Hata hivyo uchunguzi wa Jeshi la Polisi unaonesha kuwa madini hayo yametoka katika machimbo ya Kijiji cha Yobo Kwahemu Wilayani Chamwino, na juhudi za kuwapata washiriki na wanunuzi zinaendelea ili kuweza kuwafikisha Mahakamani.

“Katika mahojiano na mtuhumiwa yeye amekiri kuwa madini hayo ni yake ila hana leseni ya kuchimba madini wala leseni ya biashara wala ile ya kusafirisha madini, sasa tunafanya msako kuwabaini washirika wake tuweze kuwafikisha katika vyombo vya sheria.” Aliongeza Kamanda Muroto.

Akiongea na Dar 24 ili kupata ufafanuzi juu ya taratibu husika za usafirishaji madini, Mhandisi Migodi wa Ofisi ya Madini Dodoma Sasi Marwa, amesema muhusika alipaswa kuwa na vibali toka eneo husika na kwamba tahmini itafanywa ili kujua thamani halisi ya madini hayo.

Tukio hili linakuja ikiwa ni siku moja baada ya Jeshi la Polisi Mkoani Dodoma, kuwakamata watu zaidi ya 70 kwa makossa mbalimbali, ikiwemo usafirishaji wa mafuta ya vyombo vya moto kwa njia hatarishi.

Neymar Jr adhihirisha ujabari
Magufuli atangaza siku 7 za hekaheka, Vigogo 10 wakalia kuti kavu