Serikali ipo katika harakati za kuyatumia mawimbi ya runinga kufikisha huduma ya mawasiliano ya intanet kwa maeneo hasa ya vijijini ili wananchi wapate fursa mbalimbali za kimitandao ikiwepo upataji wa taarifa kwa wakati.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya Waziri wa ujenzi, uchukuzi na mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe kukagua mnara wa mawasiliano mjini Kondoa ambao umefungwa vifaa maalumu vya kubeba mawimbi ya runinga na kubadilishwa kwa ajili ya matumizi ya huduma ya intaneti kwa shule ya Sekondari na chuo cha ualimu Bustani mjini hapo.

Kamwelwe amekagua teknolojia hiyo kabla ya kufunga Kongamano la nne la mtandao wa intaneti kwenye Jamii lililofanyika kwa siku 6 chuo kikuu cha Dodoma (UDOM) na shule ya sekondari ya wasichana Kondoa lililoanza Oktoba 28 na kumalizika Novemba 2, 2019.

Akiwa mahali hapo Mkufunzi Msaidizi wa chuo kikuu cha Dodoma (UDOM), Jabhera Matogoro amemweleza Waziri Kamwelwe kuwa mawimbi kwa ajili ya runinga yanasafiri umbali wa kipenyo kizichozidi kilomita ishirini ambapo baadhi ya maeneo hayafikiwi kutokana na kiasi kikubwa cha mawimbi kutotumika ipasavyo.

“Ni kiasi kidogo cha mawimbi haya ndicho kinatumika kwa ajili ya kurusha matangazo ya runinga na mawasiliano ya simu za mkononi lakini mawimbi mengi yanapotea kwakua hakuna watumiaji wa huduma hii wa kutosha,” amebainisha Matogoro.

Amesema katika utafiti wake amebaini kuwa mawimbi hayo yanaweza kubadilishwa kwa kutumia vifaa maalumu kwa kuzingatia ukuaji na maendeleo ya teknolojia ambapo mawimbi ya luninga yanaweza kutumika kupeleka huduma ya intaneti katika jamii husika.

“Lengo kuu ni kuunganisha jamii na wananchi ambao hawajaunganishwa na mtandao wa intaneti kwa kutumia mawimbi ya runinga lakini yanasafiri umbali wa kipenyo kizichozidi kilomita ishirini na baadhi ya maeneo hayafikiwi,” amefafanua Matogoro.

Baada ya maelezo hayo Waziri Kamwelwe amempongeza Matogoro na kubatiza utafiti wake jina la “Teknolojia ya Matogoro” kwa kuwa amebuni kitu hicho kwa kutumia mawimbi ya runinga kupeleka huduma ya intaneti kwenye jamii na kumuahidi kuwa Serikali itahakikisha teknolojia hiyo inatumika na kuenea sehemu mbali mbali nchini.

“Nitakaa na taasisi na wataalamu ili ikibidi tuzibadilishe sera zetu kanuni zetu na utaratibu ili kuhakikisha kuwa mnaendelea kuongeza matumizi ya mawimbi ya runinga kutoa huduma ya intaneti kwenye jamii hasa kwa maenwo kama haya” amesisitiza Kamwelwe.

Kufuatia hatua hiyo Waziri Kamwelwe ameuelekeza uongozi wa UDOM kuwasilisha maombi rasmi ofisini kwake ili waweze kupewa kibali kwa ajili ya utafiti wa mtaalamu wao kuendelea kutumia mawimbi hayo kutoa huduma ya intaneti kwenye taasisi hizo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Dkt. Maria Sasabo amesema maelekezo ya Waziri yamezingatiwa na kuhakikisha wanafanyia kazi maagizo hayo ili kuendelea kuchangia maendeleo ya taifa na kuwezesha utoaji na upatikanaji wa huduma za mawasiliano.

Kongamano hilo limehudhuriwa na wataalamu wa taasisi za Serikali na binafsi 135 kutoka nchi 18 ikiwemo Argentina, Canada, Hispania, Uingereza, Marekani, DRC Congo, Cameroon, Ethiopia, Kenya, Malawi, Namibia, Nigeria, Afrika Kusini, Uganda, Zimbambwe, Ujerumani, Ufaransa, na wenyeji Tanzania.

Masauni alia na wananchi wanaoozea jela
Majaliwa azitaka AZAKI kuielimisha jamii ulipaji kodi