Muamuzi Ruddy Buquet jana alilazimika kusimamisha mchezo wa ligi daraja la kwanza nchini Ufaransa kati ya Olympic Marseille dhidi ya Olympic Lyon, baada ya mashabiki wa timu mwenyeji kuanzisha fujo katika dakika ya 62.

Mashabiki wa Olympic Marseille walianzisha zogo kwa kurusha chupa, mafataki pamoja na mabaki ya vyakula sehemu ya kucheleza hali ambayo ilileta taharuki kwa wachezaji pamoja na mashabiki wa timu pinzani.

Kutokana na hali hiyo muamuzi alilazimika kupuliza kipyenga cha kusimamisha mchezo na kuwaamuru wachezaji waingie katika vyumba vya kubadilishia kwa usalama.

Askari wa kutuliza ghasia katika uwanja wa Velodrome walilazimika kuingia uwanjani wakia na vifaa vya kazi na kuanza kutuliza ghasia ambazo zilikua zinaendelea kutanda miongoni mwa mashabiki wa timu mwenyeji kwenda kwa wenzao wageni.

Sababu kubwa ya balaa hilo kutokea uwanjani hapo, limetajwa kuwa ni hasira za mashabiki wa Olympic Marseille kumuona aliyekua mchezaji wao  Mathieu Valbuena, akirejea uwanjani hapo akiwa na timu pinzani.

Hata hivyo mchezaji huyo alionesha kuwapuuza mashabiki na aliendelea kucheza soka japo alikua akipata wakati mgumu alipokua akicheza sehemu za pembeni mwa uwanja na kupiga mipira ya kona.

Pamoja na mambo hayo kujitokeza, hali ilirejea kuwa shwari na muamuzi Ruddy Buquet alizirejesha timu uwanjani na kumalizia mchezo ambao ulishuhudia timu hizo mbili zikifungana bao moja kwa moja.

Mathieu Valbuena aliihama Olympic Marseille mwaka 2014 baada ya fainali za kombe la dunia na kutimkia nchini Urusi baada ya kusajili na klabu ya Dynamo Moscow, lakini mwanzoni mwa msimu huu alirejea nchini Ufaransa na kusajiliwa na Olympic Lyon.

Mathieu Valbuena alikua mchezaji wa Olympic Marseille tangu mwaka 2006 na aliitumikia klabu hiyo katika michezo 242 na kufunga mabao 27.

Martial Ampa kiburi Louis Van Gaal
Mabasi Mengine 138 Ya Mwendo Kasi Yashushwa Dar