Mkuu wa wilaya ya Makete mkoani Njombe, Veronica Kessy ametoa wito kwa wananchi wa makete wanaoishi ndani na nje ya wilaya ya Makete kurudi nyumbani na kufanya maendeleo katika wilaya yao, kutokana na uhalisia kuwa wanamakete wengi walio na vipato nchini kuwekeza  nje ya wilaya yao.

Kessy ametoa wito huo wakati akizindua mashindano ya M.D.A super cup  yaliyofanyika uwanja wa sabasaba mjini Makete yaliyoanzishwa na chama cha maendeleo Makete M.D.A  kwa dhima ya kuhamasisha maendeleo na kutambulisha chama hicho wilayani humo kilicho chini ya wajumbe (wanamakete) wanaoishi ndani na nje ya wilaya hiyo.

“Hali niliyoiona wakati naingia Makete kwa kweli nikasema inatakiwa tufanye iwe wilaya ya kiutalii kwasababu wananchi wake wamekuwa wanahama na kwenda kufanya makazi maeneo ya nje ya Makete, nikawapa kazi M.D.A wahakikishe wenyeji waliopo nje ya Makete wanarudi Makete na kufanya maendeleo mbali mbali tunaushahidi wa kutosha matajiri wakubwa waliopo Dar es salaam kariakoo, waliopo Makambako, Mbeya,Tunduma wote ni wanamakete lakini nyumbani kunafanana na huko?” amesema Veronica Kessy

Katibu wa chama cha maendeleo Makete, Mpandila anasema moja ya malengo ya chama hicho ni kuhamasisha jamii na watu wanaotoka katika wilaya hiyo na kushindwa kukumbuka kuleta maendeleo.

“Malengo mojawapo ya chama chetu ni kuhamasisha jamii ya wanamakete ambao wakienda kuishi nje hawakumbuki nyumbani na wakileta maiti wanalala kwenye gari tumesema hiyo imetosha” amesema Mpandila.

Festo Richard Sanga ni mkurugenzi wa timu ya Singida United na mwenyekiti wa kamati ya michezo ya chama cha maendeleo Makete ambaye ameongozana na timu ya Singida United na kushiriki katika uzinduzi wa ligi ya M.D.A kwa kucheza na timu mbili wilayani humo. Amesema malengo yake ni kuona anapata vipaji kutoka Makete na tayari baadhi ya viongozi wa timu Singida United pamoja na viongozi wa wilaya wako macho kuangalia vipaji katika mashindano hayo.

Baadhi ya wananchi wilayani Makete wametoa pongezi kwa wanamakete wanaoishi nje ya wilaya yao kwa kuanza kuonyesha nia ya kurejesha maendeleo huku wakiomba chama cha maendeleo Makete kuongeza nguvu ili kumfikia kila mwanamakete aliyepo nje ya wilaya hiyo.

Mfaume Mfaume ampiga Keisi, Kiduku naye atusua kwa KO
Video: Hotuba ya Profesa kabudi yaibua gumzo Kenya, Sumaye abwagwa uenyekiti Chadema