Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, January Makamba amesema kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi 60 Duniani ambazo zimepiga marufuku suala la mifuko ya plastiki ikiwa ni sehemu ya makubaliano ya Jumuiya za Kimataifa.

Ameyasema hayo jijini Dar es salaam katika mkutano wa pamoja na viongozi wa mkoa wa Dar es salaam wakiwemo wakuu wa Wilaya na Mameya wa jiji hilo, ambapo amesema pia suala hilo limeipa sifa kubwa Tanzania.

“Tanzania ni sehemu ya Jumuiya za kimataifa waliyoingia makubaliano ya katazo la mifuko ya plastiki, mpaka sasa ni nchi 127 zimeshajaribu kuchukua hatua, na nchi 60 zimeshapiga marufuku moja kwa moja matumizi ya mifuko ya plastiki,” amesema Makamba.

Aidha, amesema kuwa Tanzania imeingia mfumo wa Kimataifa, mashirika yote ya Ndege yanayokuja Tanzania na mashirika ya kiutalii yanayokata tiketi kwa abiria wa Tanzania, wanatoa tangazo kuwa Tanzania mifuko ya plastiki haikubaliki, limetupa heshima kubwa.

Amesema kuwa badala ya jambo hilo kuonekana kuwa litatikisa uchumi, uzalishaji na kodi, limeonekana kuwa ni jambo ambalo litaibua uchumi mpya na maendeleo kwa wananchi, huku akiwaondoa hofu wananchi.

Kuanzia Juni 1, 2019 Serikali inatarajiwa kuanza kutumia sheria ya upigaji marufuku ya mifuko ya plastiki kufuatia kukamilika kwa kanuni zake.

Habari Picha: JPM awasili nchini Namibia
Majaliwa atoa onyo kwa wamiliki wa vituo vya watoto yatima