Jeshi la maji la Marekani limedai kuwa limeitungua ndege ya kivita ya Iran isiyo na rubani (drone) iliyokuwa katika anga lake kwenye ukanda wa Hormuz, Alhamisi, Julai 19, 2019.

Rais Donald Trump ameeleza kupitia mtandao wa Twitter kuwa jeshi la Marekani liliishambulia na kuiharibu ndege hiyo ambayo ilipita takribani hatua 1,000 karibu na meli yao ya kivita.

Taarifa hiyo ya shambulizi imekuja wakati ambapo kuna taharuki iliyozuka kati ya Washington na Tehran kufuatia kutoelewana kuhusu makubaliano ya mradi wa kinyuklia wa Iran.

“Ndege hiyo isiyo na rubani ilikuwa inatishia usalama wa meli yetu ya kivita na wafanyakazi wa meli na iliharibiwa mara moja,” alisema.

“Hiki ni kitendo cha hivi karibuni cha uchokozi dhidi ya meli za kimataifa kianachofanywa na Iran. Marekani ina haki ya kulinda watu wake na mali zake pamoja na maslahi yake,” aliongeza Rais Trump.

Hata hivyo, Iran imekanusha taarifa hizo na kueleza kuwa hakuna ndege yake yoyote ambayo imetunguliwa.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Seyed Abbas Araghchi alieleza kupitia mtandao wa Twitter akikanusha maelezo ya Marekani akidai kuwa huenda waliishambulia ndege yao wenyewe.

“Hatujapoteza ndege yoyote katika eneo la Hormuz au eneo lolote duniani. Hofu yangu ni kwamba huenda Marekani wameshambulia ndege yao wenyewe,” tafsiri ya Kiswahili isiyo rasmi ya ujumbe wa Waziri Seyed.

Katika tamko lake kwa vyombo vya habari, Jeshi la Iran limeeleza kuwa ndege yake ya kivita ilifanya ukaguzi katika maeneo yake na kurejea salama.

Sakata la ufisadi Ikulu, Zuma agoma kuhojiwa
Makampuni ya Ulinzi yanayo ajiri vikongwe hatarini kufutwa