Mashambulizi yaliyofanywa na vikosi vya Marekani nchini Somalia yamefyeka ngome ya mafunzo ya kundi la kigaidi la Al-Shabaab, eneo ambalo wahitimu wapya walikuwa wanajiandaa kuanza kazi ambapo makumi waliuawa.

Hayo yameelezwa na maafisa wa kiintelijensia wa Somalia, walipokuwa wanatoa taarifa ya kipindi cha mwaka mmoja wa mashambulizi dhidi ya kundi hilo la kigaidi lenye uhusiano na Al-Qaeda.

Maafisa wawili wa jeshi la Somalia wameliambia Shirika la Habari la Associated Press kuwa makombora kadhaa yalifyatuliwa Ijumaa iliyopita na ndege za Marekani zisizo na marubani zikilenga wapiganaji wa kundi hilo.

Imeelezwa kuwa baadhi ya wapiganaji waliokuwa kwenye mafunzo ya Al-Shabaab walichomwa hadi kufikia hatua ya kutotambuliwa, zaidi ya wapiganaji 75 walifyekwa.

Kikosi cha Marekani kilichoshirikiana na majeshi ya Umoja wa Afrika kimeeleza kuwa mashambulizi hayo yalifanywa kwa lengo la kuhakikisha kundi hilo lenye uhusiano na Al-Qaeda haliendelei kustawi.

Al-Shabaab wana maelfu ya wapiganaji na wamekuwa wakifanya mashambulizi ya kushtukiza pamoja na matukio ya kujitoa mhanga dhidi ya maafisa waandamizi wa Serikali ya Somalia na kufyatua vilipuzi katika maeneo mbalimbali ndani ya nchi hiyo pamoja na nchi jirani ya Kenya.

Kundi hilo pia limekuwa likifanya mashambulizi ya kushtukiza dhidi ya vikosi vya Marekani, Umoja wa Afrika na Serikali ya Somalia.

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Oktoba 18, 2018
Mwanafunzi aua wenzake 19 kwa risasi, ajiua