Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewapa siku moja kwa viongozi wa Manispaa ya Morogoro kutenga maeneo maalumu kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo na kuyatangaza kesho.

“Mbali na kutenga maeneo pia nawaagiza muwasaidie wafanyabiashara hawa kuunda vikundi kulingana na aina ya biashara wanazozifanya ili kuwawezesha kupata mikopo kwa urahisi kutoka katika taasisi za fedha” alisema.

Majaliwa ametoa agizo hilo alipotembelea mradi wa ujenzi wa kituo cha mabasi Msamvu unaojengwa kwa ubia kati ya Manispaa ya Morogoro na Mfuko wa Pensheni wa LAPF ambapo awamu ya kwanza ya mradi huo unatarajiwa kufunguliwa Agosti 12 mwaka huu.

Mradi huo umetajwa kuwa utakuwa ni kituo cha mabasi cha kwanza cha kisasa Tanzania ambapo Waziri Mkuu amezitaka halmashauri zote zilizoko makao makuu ya mikoa nchini kuiga mfano huo.

Pia Waziri alitumia fursa hiyo kulipongeza Baraza la Madiwani la Manispaa ya Morogoro na LAPF kwa kubuni mradi huo wa kisasa utawezesha abiria kupata taarifa ya basi lilipo na muda litakapowasili kituoni hapo hivyo kupunguza udanganyifu kutoka kwa mawakala wasiokuwa waaminifu.

Katika hatua hiyo, Meneja wa mradi huo Stanley Mhapa alisema mradi huo umegharimu sh. bilioni 40 ambapo Manispaa inamiliki asilimia 40 ya hisa na mfuko wa LAPF unamiliki asilimia 60.

“Mafanikio ya mradi huu ni pamoja na kuiwezesha Manispaa kuongeza ukusanyaji wa mapato kutoka sh 350,000 kwa siku hadi kufikia sh. milioni 1.7 kwa siku,” alisema.

Mhapa alisema mradi huo utakapokamilika utatoa huduma mbalimbali ikiwa ni pamoja na huduma za kibenki, vibanda vya biashara, sehemu za chakula, ofisi na sehemu ya mapumziko ya abiria na vibanda vya kukatia tiketi.

Luis Enrique: Naamini Katika Sera Ya Kuwabadili Mara Kwa Mara
Video: Steps Entertainment yapigwa faini mil. 7, Yapewa siku 7